Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR), kupitia Mradi wa TAKeOFF awamu ya pili tarehe 20/11/2025 imefanya mkutano wa pamoja na kamati za afya za Ofisi ya Mganga Mkuu wa Mkoa wa Lindi pamoja na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa (Sokoine) ili kuzindu awamu ya pili ya utekelezaji wa mradi.
Mkutano huo umetoa fursa ya kujadili mbinu bora za kutekeleza mradi unaolenga kupambana na vikwazo vya kupambana na ugonjwa wa mabusha na matende katika mkoa wa Lindi na mikoa mingine yenye tatizo hili.
Aidha mkutano huo umejikita katika kufanya mapitio ya utekelezaji wa awamu ya kwanza na kuweka mikakati thabiti kwa awamu ya pili ya kuendelea kupunguza maambukizi katika maeneo machache yaliyosalia na pia namana ya kuwahudumia wenye madhara ya mabusha na matende.
Akifungua mkutano huo, Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Dkt. Enock S. Chilumba, aliishukuru NIMR kwa kuichagua Lindi kuwa eneo la utekelezaji wa mradi huo muhimu. Amesema kuwa mradi wa TAKeOFF awamu ya kwanza umesaidia kuibua wagonjwa wa maradhi ya mabusha na matende zaidi ya 4,000 na kwamba wagonjwa 3,571 walipatiwa matibabu kupitia Mpango wa Taifa wa Kutokomeza Magonjwa Yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele (NTDCP) kwa kushirikiana na wadau wengine wa afya.
“Kuwepo kwa NIMR Lindi ni fursa kubwa wanatusaidia kuwajengea uwezo watumishi wetu katika nyanja za utafiti na kuhakikisha tafiti zinakamilika kwa wakati na kuleta majibu yatakayoboresha huduma za afya,” alisema Dkt. Chilumba.
Kwa upande wake, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Lindi – Sokoine, Dkt. Alexander Makalla, alisema kuwa majadiliano hayo yatasaidia kuzalisha nyaraka muhimu zitakazotumika kama mwongozo katika utoaji wa huduma kwa wagonjwa wa mabusha na matende.
“Sisi kama Hospitali na wadau wengine tuko tayari na tumejipanga, msisite kutushirikisha pale mnapohitaji mchango wetu ili mradi huu uzalishe matokeo chanya,” alisisitiza Dkt. Makalla.
Akizungumza katika mkutano huo, Mtafiti Mkuu wa Mradi wa TAKeOFF, Dkt. Akili Kalinga, alisema kuwa lengo la kikao ni kushirikisha wadau muhimu katika hatua za mwanzo za mradi ili kuhakikisha kila upande una uelewa na ushiriki wa pamoja. Ameeleza kuwa Lindi ni miongoni mwa mikoa yenye maambukizi makubwa, hivyo ni muhimu kuimarisha jitihada katika awamu hii ya pili.
Katika mkutano huo, jumla ya tafiti tano ziliwasilishwa, ambazo zinatekelezwa chini ya mradi kuanzia mwaka 2024 hadi mwaka 2027, ambazo ni utafiti unaohusu Kulinganisha ubora wa mifumo ya kupima na kutibu kwa dawa ya ‘Doxycycline’ au ‘Moxidectin+Albendazole’ kwa kufananisha na Kingadawa ya ‘Ivermectin+Albendazole’ inayogawiwa kwa jamii kusaidia kutokomeza ugonjwa wa Matende na Mabusha nchini Ghana na Tanzania – Hatua ya 3 ya majaribio ya dawa katika mikoa ya Mtwara Lindi na Tanga, utafiti unaohusu Tathmini ya Maambukizi na changamoto kuelekea kutokomeza ugonjwa wa Usubi Tanzania: uzoefu wa eneo la maambukizi la Ruvuma baada ya zaidi ya miongo miwili ya ugawaji wa Kingatiba kwa jamii.
Tafiti zingine zilizowasilishwa ni Ufuatiliaji wa maradhi ya Matende na Mabusha na jinsi ya kuyatolea taarifa kwa kuwatumia watoa huduma za afya wa jamii ili wagonjwa waweze kupata huduma za kupunguza madhara na kuzuia ulemavu katika vituo vya kutolea huduma za afya, Utafiti wa kuangalia Uhusiano kati ya magonjwa yasioambukiza (NCDs) na magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele (NTDs) na utafiti wa Utambuzi wa vimelea vinavyosababisha homa za mitoki (ADL) kwa wagonjwa wa matende yanayosababishwa na minyoo ya Filaria.
Mkutano huo wa siku moja uliofanyika Lindi umewakutanisha wadau wa afya ikiwamo kamati za afya za Ofisi ya Mganga Mkuu wa Mkoa wa Lindi pamoja na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa( Sokoine), Watafiti na watumishi wa NIMR.
Section Title
Lorem ipsum dolor sit amet, consectetur adipiscing elit. Ut elit tellus, luctus nec ullamcorper mattis, pulvinar dapibus leo.









