Wanawake wa NIMR Mbeya Waadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanawake kwa Matendo ya Huruma na Elimu ya Uwiano wa Majukumu ya Kazi na Familia.
Katika kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanawake Duniani, tarehe 08 Machi, wanawake wa Taasisi ya Taifa ya Magonjwa ya Binadamu (NIMR) Kituo cha Mbeya walionyesha mshikamano na kujitolea kwa jamii kupitia shughuli mbalimbali za kijamii, matendo ya huruma, na utoaji wa elimu, wakilenga kuimarisha ustawi wa wanawake na makundi yenye uhitaji maalumu. Maadhimisho haya mwaka huu yalibeba kaulimbiu isemayo: “Haki ya Mwanamke na Wasichana, Msingi wa Maendeleo Jumuishi Kufikia Dira 2050.”Maadhimisho hayo yalianza kwa ziara ya kipekee katika kituo cha watoto yatima cha Mountain Glory, kilichopo Pambogo, kata ya Iyela. Watumishi wa NIMR Mbeya walitoa msaada wa vyakula, nguo, na mashine ya kufulia nguo, ili kusaidia kuboresha maisha ya kila siku ya watoto waliokuwa katika kituo hicho.Pia, wanawake hao walitembelea Kituo cha Afya Ruanda kilichopo jijini Mbeya, ambapo walikabidhi mashuka kwa ajili ya wodi ya wazazi. Msaada huo unatarajiwa kuboresha huduma na mazingira ya wagonjwa, hususan akina mama wanaojifungua katika kituo hicho.Siku ya kilele ilijaa elimu na mafunzo. Madaktari na watafiti wa NIMR Mbeya walitoa elimu kwa wanawake kutoka taasisi mbalimbali kuhusu umuhimu wa tafiti za afya na nafasi ya wanawake kushiriki kikamilifu katika tafiti hizo. Lengo lilikuwa kuongeza uelewa na kuhamasisha wanawake kuwa sehemu ya maendeleo ya sayansi na afya katika jamii.Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, Dkt. Betrece Ngaraguza aliwafundisha wanawake namna ya kuweka uwiano kati ya majukumu ya kazi, familia, na jamii bila kuathiri afya zao. Alisisitiza kuwa kupanga majukumu kwa uangalifu ni muhimu kulinda afya za kimwili na kiakili.Kwa upande wake, Dkt. Lucy Mrema alitoa mada kuhusu uhusiano kati ya biolojia ya mwanamke na maisha ya kisasa, akisisitiza jinsi maarifa haya yanavyosaidia wanawake kupanga kwa ufanisi kazi, maisha binafsi na familia huku wakihakikisha afya zao zinadumishwa.Naye mlezi wa wanawake wa NIMR Mbeya, Bi. Mwanaharabu Gwato, alisema shughuli hizi ni sehemu ya utamaduni uliojengeka miongoni mwa wanawake wa taasisi hiyo. Alibainisha kuwa wanawake wa NIMR Mbeya wamekuwa na desturi ya kuangalia na kusaidia jamii zenye uhitaji maalumu kama njia ya kurejesha mchango kwa jamii.Maadhimisho haya yamethibitisha kuwa wanawake si tu nguvu kazi katika utafiti na maendeleo ya afya, bali pia ni nguzo muhimu katika kuimarisha ustawi wa jamii kupitia elimu, huduma, na mshikamano. Lorem ipsum dolor sit amet, consectetur adipiscing elit. Ut elit tellus, luctus nec ullamcorper mattis, pulvinar dapibus leo.

